Header Ads

“Kagera Sugar itapata ushindi wa kwanza dhidi Yanga”-Nahodha Kavila


Kwa wale wafuatiliaji wa VPL wanajua kwamba, Kagera Sugar bado haijashinda mchezo hata mmoja katika mechi tano ilizocheza za ligi kuu tangu kuanza kwa msimu huu. Bado wapo kwenye harakati za kutafuta ushindi wao wa kwanza msimu huu.
Kesho Jumamosi October 14, 2017 ‘Nyerere Day’ kutakuwa na bonge la mechi kwenye uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba Kagera Sugar watakuwa wakicheza na Yanga ambao ndio mabingwa watetezi wa taji la VPL. Endapo Kagera Sugar itashinda dhidi ya Yanga, utakuwa ni ushindi wao wa kwanza msimu huu (2017/2018).
Historia inaonesha Kagera hawana rekodi nzuri kwa Yanga, katika mehi tano zilizopita wamefungwa zote huku kipigo kibaya kwao kikiwa ni cha msimu uliopita kwenye uwanja wao walipokubali kulazwa 6-2 kama wamesimama. Mara ya Mwisho Kagera kupata ushindi dhidi ya Yanga ilikuwa ni 2014 miaka mitatu iliyopita.
  • 14/10/2017  Kagera Sugar ?? Yanga
  • 09/05/2017 Yanga 2-1 Kagera Sugar
  • 22/10/2016 Kagera Sugar 2-6 Yanga
  • 03/04/2016 Yanga 3-1  Kagera Sugar
  • 31/10/2015 Kagera Sugar 0-2 Yanga
  • 18/03/2015 Yanga 2-1 Kagera Sugar
  • 01/11/2014 Kagera Sugar 1-0 Yanga
ShaffiDauda.co.tz imefanya mahojiano na kiungo na nahodha mkongwe wa timu hiyo George Kavila ambaye amesema, kesho gari lao ndio litawaka moto, watahakikisha wanapata ushindi wao wa kwanza kwa Yanga.
“Mechi ni ngumu lakini naamini kesho tutapata ushindi katika ligi kwa mara ya kwanza tangu kuanza kwa ligi” anasema Kavila ambaye bado anauguza majeraha na hatokuwa sehemu ya kikosi kitakachocheza dhidi ya Yanga katika mchezo wa Jumamosi hii.
Kutokana na uzoefu wake ndani ya Kagera Sugar na ligi kuu, Kavila anasema timu yake haina tatizo lolote linalowakosesha matokeo, lakini kufanya kwao vizuri msimu uliopita, kunasababisha kupata changamoto kubwa kutoka kwa vilabu vingine vya VPL.
“Hakuna tatizo lolote lile, mambo hayo hutokea kwa timu nyingi tu, nadhani msimu huu imetokea kwetu lakini kufanya kwetu vizuri katika msimu uliopita kunafanya timu nyingi kutukamia msimu huu haya ni mapito tu naamini tutakaa sawa Mungu akipenda kuanzia kesho.”
Kuhusu kipigo kikubwa walichopata kutoka kwa Yanga msimu uliopita, Kavila amesema matokeo hayo kwa kiasi kikubwa yalichangiwa na uchovu wa safari na si vingevyo.
“Msimu uliopita Yanga walitufunga 6-2 Kaitaba kwa sababu ya uchovu wa safari na si vinginevyo, uliona tulivyokuja Dar wakashinda 2-1 la tulitoa ushindani wa kutosha. Naamini kesho tutapata pointi tatu Mungu akipenda.”

No comments