Header Ads

Mambo niliyoyaona kwenye game ya Chelsea vs Watford Stamford Bridge


Nimehatika kushuhudia mchezo wa Chelsea dhidi ya Watford mechi ambayo imemalizika kwa The Blues kushinda 4-2,watu wengi wameonesha wasiwasi kwamba huenda timu hiyo ikashindwa kufanya vizuri kufuatia kukosekana kwa kiungo wao mahiri N’Golo Kante ambaye anauguza majeraha aliyopata wakati akiitumikia timu yake ya taifa ya Ufaransa.
Mashabiki wa Chelsea hapa London hawamzungumzii sana kukosekana kwa kiungo wao Kante licha ya kwamba ni moja kati ya wachezaji mahiri na muhimu kwenye kikosi chao lakini kutokuwepo kwake inafahamika moja kwa moja kwamba kuna pengo.
Changamoto kwa Antonio Conte ni kuhakikisha timu inapata matokeo bila kujali kuna mchezaji fulani yupo au fulani hayupo, hapo ndipo inaonekana kazi na umuhimu wa kocha.
Katika siku za karibuni Chelsea imeonekana ikihangaika sana kuzua timu pinzani kwenda kwenye eneo lao la hatari kwa hiyo ukifuatilia mechi kadhaa ambazo wamecheza kwenye uwanja wao wa nyumbani ni mechi nyingi wameshindwa kumaliza bila kuruhusu nyavu zao kutikishwa. Bora wangekuwa wanaruhusu nyavu zao zitikishwe lakini mwisho wa siku wao wawe wamefunga magoli mengi kwa maana ya kwamba wameshinda mechi kama ilivyo kwa Liverpool.
Mechi zilizopita kwenye uwanja wao wa nyumbani hazikuwa zenye matokeo mazuri, mechi dhidi ya Tottenham walishinda 2-1, wakafungwa na Burnley 3-2, kilichokuwa kinazua mijadala ni kwa nini Chelsea imeshindwa kuwa na mwendelezo hasa kwenye eneo la kiungo.
Kama ilivyokuwa kwenye mechi kadhaa zilizopita, Conte amewatumia Bakayoko na Fabregas kwenye eneo la kiungo na kutengeneza mwonekano mpya wa safu ya ulinzi. Wengi tumezoea kumuona Conte akitumia mfumo wa mabeki wa tatu halafu anajaza watu wengi kwenye eneo la kiungo huku akitegemea zaidi ma-wing back wa kushoto na kulia (Victor Moses akitokea kulia) na (Marcos Alonso akitokea kushoto.)
Namna alivyotumia muda mwingi kuiandaa timu kwa kuwategemea wachezaji hao hata anapoamua kufanya rotation ya kikosi chake bado wachezaji hao wamekuwa wakicheza mara kwa mara kwa sababu ni muhimili kutokana na aina yao ya uchezaji (wanakimbia sana uwanjani) kufanya coverage kubwa ukilinganisha na mtu kama Fabregas ambaye hakimbii sana lakini anafaida zake kwa sababu mipira yake mingi haipotei.
Mbio za Moses kwenda na kurudi ni tofauti na Cesar Azpilicueta ambaye yeye kwa asili ni beki wa pembeni lakini mfumo unamfanya awe wing-back, anavyocheza Moses ni tofauti na anavyocheza Azpilicueta. Kwenye mfumo unaomfanya Moses acheze, Azpilicueta anacheza ndani kwa hiyo kutokuwepo kwa hawa mabwana (Moses na Kante) kunabadili tempo na rhythm ya timu.
Kwa mfano leo nimemuona David Luis mwanzoni alikuwa kama mtu wa mwisho katikati huku Cahill akiwa ame-focus sana kushoto wakati Antonio Rüdiger yeye alikuwa makini zaidi na upande wa kulia halafu ma-wing back walikuwa Azpiticueta na Alonso, kwenye eneo la kiungo Fabregas alikuwa mbele kati ya wale watano wa katikati.
Tofauti ya Fabregas na Kante unakuja kuiona hapa, Fabregas anapoza mchezo kwa sababu yeye sio mtu wa mbio wala kupiga mipira za harakaharaka, anachokifanya ni kupokea mipira kisha kuanzisha mashambulizi kwa hiyo kulikuwa na kuchelewa kutoka mbele ya mabeki watatu kwenda mbele kwenye eneo la kushambulia hiyo inawafanya wapinzani kuziba mianya ambayo kwa aina ya uchezaji wa Chelsea hupiga mipira yao kwenye mianya hiyo  kwa hiyo ikishazibwa wanajikuta wanapiga pass karibukaribu kitu ambacho wapinzani wao wakipata mpira wanawakimbiza ndio maana utaona walitangulia kufungwa.
Baada ya kuona wako nyuma 2-1 kipindi cha pili Conte akafanya mabadiliko ya kiufundi kwa kumtoa Alonso na kumuingiza Willian kisha kumbadilisha Azpilicueta kwenda kushoto na kucheza kama wing-back wa kushoto kisha kumrudisha kulia Pedro kuja kucheza kama wing back na kumwachia nafasi Hazard kutlia halafu Bakayoko akarudi chini Fabregas akasogea mbele.
Wakati huo Conte akamuingiza Michy Batshuayi baada ya Morata kuonekana kama alikuwa anakimbiakimbia kwa sababu hakuwa anapata mipira mingi mizuri. Na kama ulifuatilia, mipira mingi mirefu kwa namna Chelsea walivyokuwa wanacheza Watford walikuwa wanakaba mshambuliaji mmoja kwa mabeki wawili, kwa hiyo ukipiga mpira mrefu wale mabeki wawili wanamvuruga mshambuliaji na kumfanya akose nafasi kuukimbilia mpira uliopigwa mbele yake.
Kuingia kwa Batshuayi kuliisaidia timu kutokana na nguvu zake, composure, ubunifu ukaongezeka kwa sababu mipira mbingi ikawa inaenda kwa Hazard na Pedro ambao walikuwa upande mmoja kushoto unamkuta Azpilicueta na Willian kwa hiyo timu ikabadilika tofauti na ilivyokuwa imeanza mwisho wa siku wakatengeneza nafasi za kutosha na kufunga magoli yaliyowafanya washinde mechi.

No comments