Header Ads

Nini kinaendelea Chelsea?Conte hana mvuto?Au Mrussi anabana matumizi?


Usajili barani Ulaya bado unaendelea, vilabu vinapigana vikumbo sokoni kutafuta wachezaji mahiri kwa ajili ya msimu ujao wa ligi na kila klabu inahangaika kununua wachezaji wakubwa na wazuri kwa ajili ya mapambano.
Hali katika klabu ya Chelsea sio nzuri hata kidogo, kama unakumbuka baada ya msimu kuisha tu ziliibuka tetesi kuhusu Antonio Conte kutaka kuondoka katika klabu hiyo huku bajeti ndogo ya usajili ikiwa moja ya sababu za kumuondoa.
Arsenal wana Lacazette tayari,United wana Lukaku,Man City wana Bernardo Silva,Liverpool wana Salah,Chelsea pamoja na tishio la kumpoteza Diego Costa lakini hadi sasa hawana jina kubwa walilonunua au wanalokaribia kununua.
Zimepita wiki kadhaa na sasa suala la bajeti ndogo kwa Chelsea linaonekana waziwazi kwani hadi sasa wameshindwa kununua wachezaji karibia wote waliokuwa wakitajwa katika list yao ya juu ya manunuzi.
Romelu Lukaku, dunia nzima iliamini baada ya mkataba wake na Everton kuisha angerudi Chelsea, Lukaku alionekana kuipenda Chelsea na ilionekana ni ngumu kuacha kutua darajani ukizingatia kwamba mustakabali kati ya Diego Costa na klabu hiyo haujakaa vizuri.
Pasipo kutarajia Manchester United walijitokeza na wakatajwa kwa muda mfupi sana na ikashuhudiwa Chelsea wakipokonywa tonge mdomoni na Lukaku akasaini Manchester United,usajili uliowaumiza sana mashabiki wa Chelsea.
Leornado Bonucci ameshasaini Ac Millan, huyu naye ilikuwa ni target ya Antonio Conte kwa muda mrefu lakini klabu ya Chelsea wameshindwa kumshawishi mlinzi huyu kujiunga nao.
Usajili wa Bonucci kwenda Ac Millan ukaleta balaa lingine kwa Chelsea ambao walimtaka sana mlinzi wa Juventus Alex Sandro lakini kuondoka kwa Bonucci kunaaminisha kwamba Juventus hawawezi kumuachia Sandro.
Antonio Rudiger amesaini Chelsea lakini ukiangalia usajili wake ulikuwa mrahisi sana kwa sababu Rudiger hakuwa anahitajika sana kwenye timu nyingine kama ilivyo kwa Lukaku,Bonucci au Sandro huku usajili wa Bakayoko nao ukiwa haueleweki.
Chelsea wanaonekana kupata tabu sana katika usajili tangu ujio wa Conte darajani, Conte analalamika kuhusu kiasi cha pesa kinavyotolewa kwa ajili ya usajili wa wachezaji wapya, jambo ambalo linawezekana kuwa kweli.
Lakini mtoa pesa huyu huyu anayelalamikiwa na Conte ndio kati ya matajiri wanaoogopwa katika manunuzi ya wachezaji, hii inaleta kigugumizi kuelewa tatizo haswa ni mvuto wa Conte au Mrusi Roman Abromovich naye anababa matumizi kama Anko Magu?

No comments