KIBA AMPONZA DIMPOZ
Alikiba na Ommy Dimpoz.
DAR ES SALAAM: Msanii Grade One Bongo, Ali Saleh Kiba ‘Alikiba’amemponza msanii mwenzake, Omary Nyembo ‘Ommy Dimpoz’ baada ya kumsababishia kuandamwa upya na ile skendo ambayo iliibuliwa mwishoni mwa mwaka jana ya kwamba jamaa ni shoga, Ijumaa linakudondoshea hii ya moto.
DIMPOZ NA USHOGA
Mwaka jana, watu f’lani wakiwa na sababu walizozijua wenyewe waliibua madai mazito kuwa, Dimpoz ni shoga lakini hakukuwa na ushahidi wowote wa kuthibitisha hilo. Hata hivyo, kutokana na kutokuwepo na vielelezo vya kuthibitisha madai hayo, skendo hiyo haikushika kasi na hata Dimpoz alipowahi kuulizwa kuhusiana na ishu hiyo alifunguka hivi:
“Kumuambia mtu ni shoga ni maneno ambayo mtu hachaguliwi kuyasema, ninachokifanya ni kutumia busara zaidi ili nisijikute najibu halafu nikaharibu.
“Ili mradi unajua kabisa wewe ni nani na unafanya nini haiwezi kukuumiza. Na lazima pia uwe mstaarabu kwa sababu unaweza kutumia kitu hasira, ukapaniki ukajikuta wewe ndiye unaenda nje ya mstari kabisa.”
Ommy Dimpoz.

YAIBULIWA UPYAA

Hata hivyo, katika hali ya kushangaza, hivi karibuni baada ya Ommy Dimpoz kutangaza kujiunga na lebo ya Rockstar4000 ambayo Alikiba ni mmoja wa wakurugenzi, skendo hiyo iliibuliwa upya na watu walioonekana kuwa na chuki za waziwazi.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili mara baada ya Dimpoz kujiunga  na Kiba, mengi yamekuwa yakisemwa lakini wapo ambao walidiriki kusema kuwa wawili hao eti ‘ni mtu na mpenzi wake’.
“Yule jamaa siyo rikizi, kwani nani asiyejua? Kaenda kufanya kazi Rockstar kumfuata basha wake,” aliandika mmoja wa mashabiki aliyeonekana si shabiki wa Kiba wala Dimpoz huku akimalizia kummwagia sifa msanii ambaye siku za hivi karibuni ameshuka sana kimuziki.

NI TEAM PINZANI

Uchunguzi wa gazeti hili pia umebaini kuwa, wanaoishikia bango ishu ya ushoga wakimhusisha Dimpoz ni Team Pinzani ya Kiba kwa kuwa hawakufurahishwa na kitendo cha msanii huyo kujiunga Rockstar4000. Akizungumza na gazeti hili, mmoja wa wadau wakubwa wa muziki Bongo aliyejitambulisha kwa jina la Kid Dizo alisema kuwa, ameshangaa kuona watu wanaibua madai ya Dimpoz kuwa shoga kipindi hiki
ambacho anakimbiza akiwa na Kiba.
“Mimi niseme tu ukweli kwamba, napenda sana muziki wa Dimpoz tangu zamani. Kwa kifupi jamaa anajua na ndiyo maana hajawahi kushuka kimuziki. Sasa mtu anapoibuka leo na kusema jamaa ni shoga, hata jamii itamshangaa.
“Kwanza siyo maneno mapya, walishaongea watu wasiomtakia mema, wakachemka, leo hii Dimpoz kajiunga na Kiba, msanii anayefanya vizuri kwa sasa Tanzania, wamenuna, wameanza tena kumchafua. Nikuambie tu kwamba huu ni mchezo mchafu unaofanywa na watu wa Team Domo lakini hawataweza,” alisema shabiki huyo.
Alikiba.

SEDUCE ME YAKICHAFUA

Aidha, baada ya Alikiba kutoa bonge la wimbo, Seduce Me ambao mpaka juzi Jumatano ulikuwa na ‘views’ 2,600,000 kwenye Mtandao wa YouTube, Team Pinzani povu limewatoka ikiwa ni pamoja na kuwachafua memba wa Rockstar4000.
Imebainika kuwa, wimbo huo ambao unatikisa Afrika nzima umewafanya Team Pinzani kuanzisha mkakati wa kuwachafua wasanii hao mtandaoni, mazingira yanayoashiria kushindwa kupambana kimuziki.
“Unajua hii kutukanana na kuzushiana mambo yasiyo ya msingi siyo muziki, watu wapambane kisanii sasa kuna timu zikiona zimeshindwa, zinaibua mambo yasiyo ya msingi,” alisema mmoja wa mashabiki wa muziki wa Bongo Fleva aliyejitambulisha kwa jina la Fred wa Sinza.

DIMPOZ ANASEMAJE?

Katika kusikia kipi anacho cha kusema kuhusiana na madai hayo yaliyoibuliwa ya ushoga hasa baada ya kujiunga na Rockstar4000, Dimpoz ambaye sasa hivi anafanya fresh na wimbo wake wa Cheche alisema:
“Tunachokifanya sisi ni kutoa ngoma kali, hayo maneno yameongewa sana lakini kwa mwenye akili timamu anajua kuwa huo ni mchezo mchafu wenye lengo la kunichafua tu. “Rockstar4000 ni lebo kubwa ya muziki Afrika, tunatoa ngoma kali na tunakimbiza, sasa wanaokomalia mambo ya ushoga wao waendelee, sisi tunapasua anga,” alisema Dimpoz ambaye hivi karibuni aliungana na Kiba katika safari ya Marekani kwenye Tamasha la One Africa Music Festival.

KIBA ATIA NENO

Gazeti hili pia lilipata fursa ya kupiga stori na Alikiba kusikia ana lipi la kusema kutokana na manenomaneno yanayozungumzwa juu ya Dimpoz ambapo alisema: “Ishu ni muziki mzuri, hayo maneno yasiyo na msingi tuyapuuze. Kikubwa mashabiki wetu wasapoti kazi zinazofanywa na Rockstar4000, Seduce Me inabamba na nyingine zinakuja.”
STORI: MWANDISHI WETU| IJUMAA