Header Ads

Tetesi za usajili: Mastaa wa kimataifa kutemwa Simba




KLABU ya Simba inatarajia kuwatema baadhi ya mastaa wake wa kimataifa ili nafasi zao kuchukuliwa na wachezaji wa Yanga, Donald Ngoma na Haruna Niyonzima.
Taarifa kutoka ndani ya Simba zinasema kuwa wachezaji hao wanakaribi kuanguka wino wa miaka miwili kwenye klabu hiyo yenye makao yake Msimbazi, Dar es Salaam.
Shaffihdauda.co.tz. imezungumza na kiongozi wa ya Simba kwa sharti la kutotajwa jina, ambaye amesema klabu hiyo inatarajia kuwanasa Haruna Niyonzima na Donald Ngoma kabla ya mwezi Julai mwaka huu.
“Tuko mbioni kukamilisha usajili wa Ngoma na Niyonzima ambao wanaweza kusaini miaka miwili, tunaendelea kupambana na kama wakisaini itabidi tupunguze wachezaji wakimataifa tuliokuwa nao msimu uliopita.”
Simba imekuwa ikiwawania Ngoma na Niyonzima tangu msimu uliopita ambapo sasa imeonekana kukaribia kuwanasa wote wawili kutokana na mikataba yao kufikia ukingoni.
Wekundu wa msimbazi hao wamemaliza Ligi Kuu ya Tanzania Bara msimu huu wakiwa nafasi ya pili nyuma ya Yanga baada ya kuvuna pointi 68 kwenye michezo 30 waliyocheza.
Sheria za Ligi Kuu ya Tanzania Bara zilizowekwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), zinaruhusu klabu za Ligi Kuu kusajili mwisho wachezaji saba wa kigeni. Hadi sasa timu hiyo ina wachezaji saba wa kigeni iliyowatumia kwenye msimu uliopita ambao ni kipa Daniel Agyei (Ghana), Method Mwanjale (Zimbabwe), James Kotei (Ghana), Janvier Bokungu (Congo DRC), Juuko Murshid (Uganda), Fredrick Blagnon (Ivory Coast) na Laudit Mavugo (Burundi).

No comments